Utakatifu
ni hija ya maisha inayotekelezwa hatua kwa hatua kama walivyofanya
Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II watakaotangazwa kuwa
watakatifu, Jumapili ijayo kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro mjini Vatican. Huu ndio utakatifu ambao watu wanaendelea
kuushuhudia katika maisha na utume wa Wenyeheri hawa.
Padre
Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican akiwa ameambatana na wahusika
wakuu katika mchakato wa kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane
Paulo II kuwa watakatifu: Padre Giovangiuseppe Califano pamoja na
Monsinyo Slawomir Oder, Jumanne, tarehe 22 Aprili 2014, wamepembua maana
ya utakatifu mintarafu maisha ya wenyeheri hawa wawili.
Yohane
XXIII katika maisha yake kama Padre, Askofu na Khalifa wa Mtakatifu
Petro alijiwekea nadhiri ya kuwa karibu na Yesu, kujificha katika Moyo
wake Mtakatifu, Kusali Rozari na kumpatia nafasi ya pekee katika maisha
yake. Haya ni mambo yaliyojionesha kwa namna ya pekee katika maisha na
utume wake kama Mchungaji na Baba.
Ni kiongozi aliyeyasimika
maisha yake katika furaha na ukarimu kiasi cha watu wengi kumwita kuwa
ni Papa mwema! Alikazia umuhimu wa mshikamano katika maisha na utume wa
Kanisa kwa kuitisha Sinodi ya Jimbo kuu la Roma na Mtaguso mkuu wa Pili
wa Vatican. Ni kiongozi aliyeonesha upendo na uelewa katika shughuli za
kichungaji; akawa kweli ni mtu wa msamaha na faraja kwa wote
waliomkimbilia. Alikazia utii na amani ya kweli duniani.
Monsinyo
Slawomir Oder anasema, utakatifu wa Mwenyeheri Yohane Paulo II ulianza
kuonekana tangu alipokuwa bado Chuo Kikuu, kiasi kwamba, baadhi ya
wanadarasa wake waliandika chumbani kwake, "Mtakatifu mtarajiwa",
kutokana na na moyo na bidii ya sala, tafakari ya Neno la Mungu na
maisha adili. Yote haya yalimwilishwa kwa njia ya matendo ya huruma.
Alikuwa
na Ibada ya pekee kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa, akawa na
ujasiri wa kukabiliana na changamnoto za maisha kwa imani na matumaini
pasi na kukata tamaa, kwani daima aliuona mkono wa Mungu ukiyaongoza
maisha yake! Watu wengi walitambua kuwa kweli Yohane Paulo II alikuwa ni
mtu wa Mungu aliyekuwa ni chemchemi ya maisha yake yote, kiasi cha
kujikita katika Uinjilishaji Mpya, ili wote waweze kuwa ni watakatifu
kwa kuonja huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao.
Tunaendelea
tena katika tafakari yetu masomo Dominika ya II ya Pasaka mwaka A. Ni
kipindi cha furaha kwa sababu ya ushindi dhidi ya kifo kwa njia ya
ufufuko. Neno la Mungu, linakazia na kuahidi furaha ya kweli kwa wale
ambao hata kama hawakumwona Bwana wanayo imani na tumaini la kweli
katika yeye.
Katika
Somo la kwanza, kutoka katika kitabu cha Matendo ya Mitume latuonesha
furaha na tabia ya jumuiya ya kwanza ya Yerusalemu. Kwa nini tunaoneshwa
jambo hilo? Ni kwa sababu tunaalikwa kuishi mtindo uleule wa jumuiya ya
mwanzo katika mazingira yetu. Mambo msingi ya Jumuiya ya I yalikuwa
utii na usikivu wa watu kwa Neno la Mungu lililohubiriwa na Mitume.
Aidha waliweka mali yao na moyo wao pamoja kwa faida yao na kasi ya
Injili.
Ili kuimarisha mambo haya waliadhimisha pamoja Ekaristi
Takatifu na kusali pamoja kwa upendo. Mambo haya msingi yalifungamana na
furaha, uchangamfu, ushirikiano ambavyo vilikuwa vivutio kwa jumuiya
nyingine nje ya Yerusalemu. Ndiyo kusema waliishi na kukishuhudia kile
walichohubiri katika maisha yao, yaani waliuishi ufufuko ambao ndilo
chimbuko la haya yote.
Mpendwa msikilizaji, wito kwetu hivi leo
katika jumuiya zetu ni kuanza polepole kupalilia nguvu ya ufufuko, ndiyo
kusema tunaalikwa kushuhudia daima kwa maisha yetu yakuwa Kristu ni
mfufuka. Mpendwa, katika mantiki hiyo katika jumuiya zetu lazima tabia
za jumuiya ya kwanza zijitokeze na kukua na hivi kuwa kielelezo cha
mapendo kwa watu wa mataifa. Yafaa kukomaza ile tabia ya kushirikishana
tulichonacho hata kama ni kidogo. Tujifunze kuwa na kile kinachotufaa na
kinachobaki kiwe kwa ajili ya wale waliowahitaji katika jumuiya zetu.
Kumbuka
usemi wa Mtakatifu Basil akisema “kama mmoja wetu angechukua kwa ajili
yake kinachohitajika na kingine kikawa kwa ajili ya ndugu yake maskini,
basi kusingekuwa na tajiri wala maskini katika jumuiya”. Hii ni falsafa
ya mgawanyo sawa ambayo tungepaswa kuifikia kama kweli tunataka kumfuasa
Bwana kwa ukamilifu! Mpendwa msikilizaji inaonekana kuna ugumu katika
kushirikishana mali tulizonazo, na hasa kuwapeni maskini, je toka
tukiamini na kuendelea katika ugumu huu twaweza kusema tunaishi na
tunashuhudia ufufuko? Tafakari sana jambo hili!
Katika somo la
Pili toka barua ya kwanza ya Mtakatifu Petro tunakumbushwa siku ya
ubatizo wetu. Kwa njia ya ubatizo tulipata kuingia katika furaha isiyo
na mwisho. Ndiyo kusema Mt Petro anataka hata kama kuna madhulumu na
taabu mbalimbali tusisahau furaha ya milele. Anasema mateso ni ya
kitambo kidogo tu na baadaye yanapita cha msingi ni kutazama mbele
tukiendelea kukua katika neema ya ubatizo.
Mtakatifu Petro
anatukumbusha kuwa mkristu katika ulimwengu huu ni mgeni na hivi yuko
safarini kwenda nchi ya ahadi yaani mbinguni. Tunakumbushwa kuwa hakuna
mateso yanayoweza kuzima moto wa furaha na mapendo uliowashwa wakati wa
ubatizo. Wakristo ni kama dhahabu ambayo ili itengeneze kitu cha thamani
lazima ipitie moto ili ichomwe na kusafishwa tayari kwa kito cha
thamani. Katika somo la Injili, hali ya maisha ya jumuiya inajionesha
wazi. Wanafunzi wako pamoja ingawa wanahofu! Bwana anawakuta wakiwa
pamoja na kuwatakieni amani. Anawaonesha alama za madonda na wanafurahi
na kusema tumemwona Bwana! Ni katika jumuiya hiyo Bwana anawavuvia Roho
Mtakatifu ili wapate kuondolea dhambi. Ni siku hii anaweka sakramenti ya
kitubio katika Kanisa na kisha anawatuma wakaende kutangaza habari
njema. Kumbe Toba ni mlango wa kazi ya kimisionari, ni mlango wa imani,
ni mlango wa wokovu. Analikabidhi kanisa ufunguo wa kufunga na kufungua
katika mambo yamhusuyo Mungu katika uhusiano wake na mwanadamu. Jumuiya
wakati fulani zinakuwa na watu walio na mashaka katika imani. Hali hii
inajionesha leo pia. Ndiyo kusema, kumbe Mtume Tomaso ambaye hakuwapo
pamoja na wenzake siku ya kwanza haamini, bado ana mashaka kuhusu
ufufuko! “Siamini mpaka nitie vidole vyangu katika makovu ya Bwana!
Baada ya siku nane tukio hilo la kitaalimungu, Bwana anawatokea tena
Mitume na wakati huo Tomaso yupo. Bwana anamwambia lete mikono yako
na uweke kidole chako katika ubavu wangu na usiwe asiyeamini! Tomaso
anajibu, Bwana wangu na Mungu wangu! Mpendwa, Mtume Tomaso anapokiri
udhaifu wake anatufundisha kuwa watu wa Imani na unyenyekevu mkubwa na
hivi baada ya ufufuko hakuna mashaka tena kinachobaki ni kwenda
kutangaza habari ya furaha kwa mataifa. Mpendwa leo hii wapo watu wa
namna hii katika jumuiya zetu, kumbe wanaalikwa na Bwana kusadiki
pasipo kuona, na kwa namna hiyo Bwana anatangaza heri kwa wasioona
wakasadiki na si kwa wanaosadiki kwa sababu ya kuona. Mwishoni mwa
sehemu ya Injili ya Dominika hii, Mwinjili anatuambia pia zipo ishara
nyingi ambazo hazikuandikwa na hivi mtu asishangae ishara nyingine
ambazo hazimo katika Biblia lakini ni muhimu kwa imani yetu na maisha ya
Kanisa. Nakutakieni furaha tele katika kipindi chote cha Pasaka na
Mungu azidi kuwa nawe, nawe ukitekeleza mapenzi yake katika Jumuiya kama
Jumuiya ya kwanza ya Waamini. Tukutane tena Dominika ijayo. Tumsifu
Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya
C.PP.S.