Mahakama
moja nchini Sudan imemkuta na hatia Meriam Yahya Ibrahim Ishaq,
mwanamke mwenye umri wa miaka 27 ya kukufuru na kuzini kwa kuwa ameolewa
na raia mmoja Mkristo kutoka Sudan ya Kusini na hivyo kuhukumiwa
kuchapwa viboko mia moja na kunyongwa hadi kufa!
Adhabu hii
imewashtua watetezi wa haki msingi za binadamu, kwa kuitaka Serikali ya
Sudan kuheshimu uhuru wa kuabudu kadiri ya Katiba ya nchi iliyotungwa
kunako Mwaka 2005.
Mahakama hiyo imetumia "Sharia" za dini ya
Kiislam zilizoingizwa nchini humo kunako mwaka 1983 zinazopiga rufuku
kwa mwamini wa dini ya Kiislam kuoa au kuolewa na Mkristo. Viongozi
mbali mbali wa Jumuiya ya Kimataifa wameitaka Serikali ya Sudan
kuingilia kati ili kusitisha utekelezaji wa adhabu hii ambayo ni kinyume
cha haki msingi za binadamu.
Ninaendelea
tena kuwa nawe katika kipindi cha Liturujia ya Neno la Mungu, tukiwa
tayari Dominika ya V ya Pasaka. Ujumbe wa Neno la Mungu umezama katika
kuamini kina katika Bwana na kisha kutoa huduma katika jumuiya kama njia
ya kukamilisha unachoamini na hivi baadaye kukuwezesha kufika mbinguni.
Bwana anaenda huko kutayarisha makao ya kutosha kwa ajili yetu.
Katika
somo la kwanza: (Mdo, 6:1-7), tunakutana na ongezeko la wanafunzi
katika jumuiya ya kwanza, na katika ongezeko hili, kunatokea malalamiko
ya Wayahudi wa Kiyunani, dhidi ya Waebrania kwa sababu ya huduma pungufu
kwa wajane. Basi Mitume wakishauriana na kusali wanaona kuwa haipendezi
wao kuacha huduma ya Neno la Mungu na kuhudumu mezani.
Uamuzi
unaotolewa ni kuwaambia wanajumuiya ya wa jumuiya ya kwanza wakisema
chagueni kati yenu watu 7 wenye karama ya wema, wenye kujawa na roho na
hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili na sisi tutadumu katika kuomba na
kuhudumia lile Neno”. Baada ya ushauri huo wakachaguliwa watu 7 kati
yao alikuwako Stefano aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, wakasali na
wakawawekea mikono na tayari wakawa mashemasi katika Kanisa.
Mpendwa
msikilizaji kwa nini kunatokea malumbano na mikingamo katika Jumuiya ya
kwanza? Kwa nini mwandishi anaweka jambo hili mbele yetu? Jambo la
kukumbuka katika simulizi hili ni kwamba hapo mwanzo Jumuiya ilikuwa na
Waebrania tu na polepole kadiri ya kazi ya kimisionari ilivyokuwa
ikisonga mbele, wakajiunga hata Wayahudi wa Kiyunani ambao walikuwa
wakitumia lugha ya Kigriki. Wayahudi wa Kiyunani walikuwa na
mchanganyiko wa tamaduni kwa maana walikuwa wakiishi nje ya Palestina.
Waebrania
ambao hawakuwa na mchanganyiko, wao waliendelea kutumia lugha ya
Kiebrania kama kawaida! Basi jumuiya ilivyozidi kuongezeka vilianza
kujitokeza vijidharau vya hapa na pale dhidi ya Wayahudi wa Kiyunani na
hasa wajane na yatima wao kuhusiana na ugawanyaji wa mali za jumuiya!
Kumbuka kuwa, tangu mwanzo walikuwa wameweka mali pamoja. Mambo haya
yalianza kujitokeza baada ya miaka 3 hivi. Kilele cha dharau ni
malumbano na madai ya kutaka Mitume washiriki katika kuhudumu mezani,
ili kuweka haki katika maisha ya jumuiya kila siku.
Basi, shauri
hilo likiwafikia Mitume, na Mitume wataamua kwa hekima ya kimungu
kuwaweka wakfu watu saba kwa ajili ya huduma hiyo. Mpendwa msikilizaji
hiki ndicho chanzo cha ushemasi katika Kanisa Moja,Takatifu, Katoliki na
la Mitume.
Mpendwa mwana wa Mungu, tunajifunza nini katika hili?
Jambo la kwanza tunajifunza kuwa tangu mwanzo Kanisa limekuwa
likikumbwa na matatizo na hivi kuonesha sura mbili za Kanisa: Kanisa la
wema na wadhambi. Kumbe hata hivi leo inapotokea purukushani fulani
katika Kanisa tusishangae, ni hali ya mwanadamu tangu mwanzo. Wajibu na
jambo la kufanya ni kusali na kuomba kwa ajili ya kupatikana suluhu kwa
njia ya amani.
Jambo la pili Mitume wametupa mfano bora yaani
wakati Kanisa linakua nao wanaona ni vema kushirikisha madaraka
waliyokabidhiwa na Mungu kwa wengine, kwa ajili ya faida ya Taifa la
Mungu. Wanapoamua jambo hili wanashirikisha jumuiya yote; huu ndio umoja
wa Kanisa, ndicho Bwana anachotaka katika kuwa mchungaji mwema. Mitume
wanabaki na lengo moja yaani utume wa Neno la Mungu.
Katika somo
la Pili: (1Mt Petro 2:4-9) Mt Petro awaalika watu wote kumwendea Yesu
Kristu jiwe hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule.
Jiwe hili ndo lile jiwe kuu la pembeni ambalo Mungu ndiye mjenzi wake.
Mungu anapojenga nyumba yake akisha kuweka jiwe kuu anasonga mbele
akitumia mawe mengine, yaani wanadamu ambao Mt Petro anasema “Katika
yeye nasi tunaitwa kuwa nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu tena
tunaalikwa kutolea daima dhabihu njema zinazokubaliwa na Mungu. Ndiyo
kusema Mungu, anajenga nyumba yake kwa kutumia mawe yaliyohai, yaliyojaa
upendo! Hawa ni wabatizwa wanaomkubali Kristu na hivi kujenga nyumba ya
kiroho yaani Kanisa la Mungu.
Mpendwa msikilizaji yafaa
kujiuliza ujenzi huu ulianza lini? Kwa hakika ujenzi umeanza wakati wa
ufufuko wa Bwana, maana waashi walilikataa jiwe hai na Mungu akalifanya
kwa njia ya ufufuko kuwa jiwe kuu la pembeni. Jambo hili lilishaaguliwa
na manabii wa kale “tazama naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni,
teule lenye heshima”. Ni kwa jinsi hiyo basi uaguzi huu umekamilika
katika ufufuko wa Bwana. Mpendwa msikilizaji kwa kuwa mawe hai ya nyumba
ya Mungu, Bwana anatuita daima kuachana na giza na tunaalikwa
kuzitangaza fadhili zake daima kwa mataifa ili waweze kuingia katika
nuru yake ya ajabu.
Katika Injili: (Yn 14:1-12) Mwinjili anaweka
mbele yetu mafundisho ya Bwana aliyoyatoa katika chakula cha jioni siku
iliyotangulia kuteswa kwake. Ndiyo kusema anawaachia wosia Mitume na
vizazi vyote. Mmoja anaweza kuuliza hivi kwa nini Mama Kanisa ameweka
somo hili baada ya Pasaka? Ni kwa sababu moja ya kawaida kwamba wosia
husomwa baada ya mwenye kuandika wosia anapokuwa ameondoka duniani!
Katika
mafundisho ya Bwana tunaona jinsi Bwana mwenyewe akiwatayarisha
wanafunzi wake kwa ajili ya Kupaa kwake. Anasema wasifadhaike bali wawe
na imani katika Mungu na yeye mwenyewe, na kisha wakumbuke anaenda
kuwatayarishia makao tele ili atakapokuwepo nao wawepo. Jambo la kwenda
kutayarisha makao linashangaza kidogo kwa sababu kuna mawazo kwamba
tayari pamekwishaandaliwa! Ni kweli, lakini ataka kutuambia suala la
kusafiri na ugumu wake linahitaji maandalizi. Kwa sababu hiyo basi,
Bwana ataongeza neno akisema huko niendako mwaijua njia!
Mpendwa
mwanatafakari, kwa kuwa njia na makao tunayopaswa kuyafikia ni kazi
nyeti, mara moja Tomaso atasema hatujui njia! Bwana mkarimu na Mchungaji
mwema anamjibu “mimi ndimi njia na ukweli na uzima; mtu haji kwa Baba
ila kwa njia ya mimi”. Hili maana yake nini? Jambo hili lamaanisha
lazima kufuata njia ya mapendo, njia ya mateso hadi msalabani na kisha
hapo kutakuwa na ufufuko.
Kumbe, matayarisho ya makao yanaanza
na msalaba wake na kisha ufufuko furaha ya milele na Baba mbinguni. Ili
tuweze kupita katika njia ya Bwana tunahitaji msaada wake na ndiyo maana
alisema, nitaenda na kisha nitarudi kuwachukua pamoja nami! Katika
kutangaza makao, Bwana ansema nyumbani mwa Baba yake, kuna makao mengi.
Bwana ataka kusema nini katika hili? Ataka kusema tukikubali kumfuasa
yeye basi kuna wajibu na shughuli za kutosha kama tuonavyo leo katika
Kanisa. Nyajibu hizi tunaalikwa kuzifanya kwa mapendo tukishirikiana
katika raha na taabu mpaka kufikia mwisho wa nyakati na hapa ndipo kuna
kumwona Baba.
Wakati Bwana anatangaza kuwa yeye ni njia ya kwenda
kwa Baba, mara moja Filipo anauliza utuoneshe Baba yatutosha! Ombi hili
linamwendea Bwana na hata sisi wakristu wa leo. Kwa upande wake Bwana
anajibu akisema aliyeniona mimi amemwona Baba, kwa kuwa mimi ni ndani ya
Baba na Baba yu ndani yangu. Kwa upande wetu tunapaswa kusema daima
aliyemwona Kristu amemwona Baba. Baada ya fundisho hilo lililo gumu
kwao, Bwana atawaalika kusadiki hilo na kama hawasadiki basi wasadikini
kwa sababu ya kazi zenyewe!
Mpendwa, kwa kumtambua na kumjua
Baba haina haja ya kujenga falsafa ya pekee bali ni kuitikia kile
ambacho Bwana anasema. Ndiyo kusema inatosha tu kumtazama Kristu yaani
Mwana, ambaye ni sura kamilifu ya Mungu. Inatosha kumtazama Mwana,
yamaanisha na yatulazimu kusoma Neno la Mungu na kutafakari, kusikia
kile anachofundisha kwa njia ya Kanisa, kupambanua namna yake ya kupenda
yaani mpende adui yako, namna yake ya kukosoa kunapokuwa na shida au
dhambi na mwishoni kuyashika yale yote mema aliyoliachia Kanisa la
Kitume.
Mpendwa msikilizaji, katika kusadiki yaani, kuamini
kuliko kina Bwana anafungamanisha zawadi, yaani anasema kama mmoja
akisadiki ataweza kufanya mambo makubwa katika maisha yake. Hili ni
kweli nami nasadiki.
Nakutakieni furaha tele katika Dominika hii
ya Pasaka na Mungu azidi kuwa nawe, ukitekeleza mapenzi yake katika
maisha yako. Tukutane tena Dominika ijayo. Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.