TAASISI ya Bilal Muslim Mission of Tanzania imewashauri Watanzania
kujitolea damu salama ili kuokoa maisha ya wengi wanaohitaji damu
hospitalini.
Ombi hilo limetolewa juzi na Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Sibtain
Meghji, alipozungumza wakati wa utoaji damu salama, tukio
lililofadhiliwa na taasisi hiyo jijini Mwanza.
Meghji alisema utoaji damu salama unatakiwa kufanywa na kila mtu
mwenye sifa ili kuisaidia jamii iliyopo hospitalini ikihitaji huduma
hiyo muhimu.
“Sote tunajua kwamba damu ni kiungo muhimu kwa mwili wa mwanadamu…
kwa hiyo mimi naomba sana Watanzania wote tujenge hulka ya kujitolea
damu mara kwa mara kwa ajili ya ndugu zetu,” alisema Meghji.
Alisema kila mwaka taasisi hiyo ya Bilal Muslim Mission of Tanzania
kwa kushirikiana na waumini wote wa madhehebu ya Shia, wanachangia
damu, ambapo jana ilitarajiwa kupata zaidi ya watu 400.
Kwa upande wake, Ofisa Uhamasishaji wa Mpango wa Damu Salama Kanda ya
Ziwa, Vincent Muhada, alisema zaidi ya chupa 40,000 za damu salama
zinahitajika katika hospitali mbalimbali za mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Alisema mahitaji halisi ya damu salama kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa ni
chupa 70,000 lakini hadi sasa chupa 25,000 hadi 30,000 zimeshapatikana,
hivyo kusababisha upungufu wa chupa 40,000.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni