Katika kuimarisha mahusiano ya kimataifa, kuimarika kwa uchumi wa nchi, uwekezaji na rasilimali za nchi nk. vyote kwa umoja wake ni biashara, hakuna ajenda itakayozungumzika karne hii kama haina maslahi ya kibiashara.
Wengine hudhani biashara inaweza kuanzishwa tu kiholela bila kuweka vigezo vinavyozingatia ubora wa bidhaa husika, wakati mwingine kutokana na unyeti wa teknolojia mpya, wachache huchukulia kama ni fursa ya kuingiza teknolojia hiyo sokoni bila kuangalia kama inakidhi viwango vya ubora.
Katika hatua za kuimarisha bidhaa zinazokubalika, Shirika la Viwango Tanzania (TBS) wiki hii lilitangaza uwepo wa vipande vya umemejua ambavyo havina ubora kwa soko la ndani, na TBS tayari limetoa tahadhari kwa wananchi kuwa makini wanaponunua vifaa vya kutengenezea mfumo huo wa umemejua.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Umma cha TBS, Roida Andusamile alisema kumepatikana taarifa za uchunguzi wa maabara uliofanywa kwa sampuli zaidi ya 10 za vipande vya umemejua ambavyo alisema vilichukuliwa vikiwa tayari madukani vikiuzwa.
Roida alisema iligundulika kuwa sampuli zote za vipande vya umemejua vilivyochukuliwa baada ya kupimwa havikuwa katika ubora unaokubalika kisheria.
Hilo ni tatizo kubwa, linahitaji mamlaka nyingine zisaidiane na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia bidhaa mbalimbali zinazotengenezwa kwa teknolojia mpya ya kisayansi ili kuthibitisha kuwa ni salama na zinakuwa katika ubora unaokubalika.
Zipo hasara kubwa mbili zinazoweza kutokea katika utumiaji wa bidhaa hafifu kama hivyo vipande husika vya umemejua, kwanza hitilafu ya umeme unaozalishwa na vipande hivyo unaweza kuathiri mfumo wa umeme unaozalishwa, na pili ni hasara ya fedha kwa kununua vipande hivyo visivyo na ubora.
Teknolojia ya kuzalisha umeme kutumia vipande vya umemejua imekua kwa haraka katika kipindi cha uhaba mkubwa wa umeme ambao ulisababisha kuwepo kwa mgawo wa umeme nchini.
Baadhi ya watu wakaamua kutumia njia mbadala ya kupata umeme, matokeo yake ni kubuni na kutengeneza vipande vya umemejua visivyo na ubora katika soko la ndani.
Hata hivyo TBS iligundua uwepo wa vipande hivyo baada ya kupewa malalamiko na watumiaji wa umemejua wakaamua kushirikiana na Taasisi ya Nishati Jadidifu (TAREA).
Baada ya kupata taarifa hizo, Roida Andusamile alisema maofisa wa wao pamoja na TAREA walishirikiana pamoja na kufanya manunuzi maalum kwenye maduka mbalimbali ya vifaa hivyo yaliyoko Kariakoo.
Roida anasema manunuzi waliyafaya kwenye mitaa ya Msimbazi na Kongo pamoja na eneo la Keko-Mwanga na kupata sampuli ambazo baada ya kuzipima wakagundua ziko chini ya viwango vya ubora.
Roida alisisitiza kuwa hata wataalam waliofanya kazi ya kuvipima vipande hivyo, waligundua uwepo wa kasoro nyingi ambazo zilisababisha vifaa hivyo viwekwe katika kundi la bidhaa zilizo chini ya viwango vya ubora.
Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti Ubora cha TBS, Ashura Kilewela alitaja maduka ambako vifaa hivyo vilinunuliwa kuwa ni Keoali Power &Equipment Co Limited, Regal Solar Limited na duka la Nishati Electronics Limited.
Kilewela alisema walichukua hatua zaidi kwa kuzuia vipande 1,321 vya umemejua visiuzwe kutoka dula la Regal Solar, na pia vipande 164 kutoka duka la Nishati Electronics kutokana na kutiliwa shaka ya ubora wake, na baadaye ilithibitika kuwa vipande hivyo ni kweli vilikuwa havina ubora.
Tunaamini kuwa jitihada za kutambua bidhaa ‘feki’ zinazoingia sokoni zitategemea ushirikiano kutoka kwa walaji watakaotoa taarifa kwa mamlaka husika kama TBS ili wao waweze kuchukua hatua stahiki.
Katika kadhia hiyo, Katibu Mtendaji wa TAREA, Mathew Matimbwi alisema kulikuwepo na kasoro nyingine katika vipande hivyo ambazo ni seli za vipande hivyo kuwa na rangi mbili badala ya moja na pia hazikuandikwa nchi zilikotengenezwa.
Maoni: 0715-047304 au owdenkyambile@gmail.com
CHANZO:
NIPASHE JUMAPILI