Week Hot newz

Jengeni utamaduni wa watu kukutana na kudumisha amani!

Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 19 Mei 2014 amekutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Mexico kwa kuwataka kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana pamoja na kujenga amani. Ili Kanisa liweze kuendelea kuwajengea watu imani na matumaini, halina budi kushikamana na wahanga wa biashara haramu ya dawa za kulevya pamoja na maskini!

Baba Mtakatifu anasema, hakuna sababu ya Kanisa kuogopa au kutishwa na nguvu za giza, bali linapaswa kusimama kidete na kwa ujasiri pamoja na watu wanaoendelea kuteseka, kwa kutetea haki zao msingi pamoja na kushiriki katika mchakato wa kuwaletea maendeleo endelevu yanayomlenga mtu mzima: kiroho na kimwili. Mambo haya yanajikita katika mchakato wa Uinjilishaji pamoja na kutafuta mafao ya wengi.