Week Hot newz

Huruma ni jina na utambulisho wa Mungu!


Huruma ni jina na utambulisho wa Mungu anasema Baba Mtakatifu Francisko. - AFP

Huruma ndilo jina na utambulisho wa Mwenyezi Mungu, hivi ndivyo anavyosema Baba Mtakatifu Francisko katika mahojiano maalum na Andrea Tornielli, mwandishi wa habari za gazeti la “La Stampa” na mhariri mkuu wa tovuti ya “Vatican insider” katika kitabu ambacho kimezinduliwa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, “Jina la Mungu ni huruma”. Kitabu hiki kimegawanyika katika sura tisa ambazo ni majibu ya maswali 40 aliyoulizwa Baba Mtakatifu Francisko kama sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu, uliozinduliwa hapo tarehe 8 Desemba 2015.
Baba Mtakatifu Francisko katika mahojiano haya anafanya rejea katika Maandiko Matakatifu, Mafundisho ya Mababa wa Kanisa pamoja na watangulizi wake, yaani Papa mstaafu Benedikto XVI, Mtakatifu Yohane Paulo II, Mtakatifu Yohane XXIII na Mwenyeheri Paulo VI. Kitabu hiki kimechapishwa katika lugha tano na nakala ya kwanza ikawasilishwa kwa Baba Mtakatifu Francisko, hivi karibuni. Kitabu hiki ni matunda ya mahojiano ya kina na majibu muafaka yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko huku akiwahamasisha waamini kutambua udhaifu wao, tayari kukimbilia huruma na upendo wa Mungu.