Kadiri ya mila za Waafrika mgeni akutembeleapo hubeba zawadi. Kwa kawaida zawadi hiyo inakuwa chakula kama vile unga katika sanduku liitwalo jamanda, linafungwa nguo nzuri na kubebwa kichwani na mwanamke, kisha mgongoni hubeba kuku kama mtoto mchanga. Afikapo ugenini, mama mwenye nyumba huzipokea zawadi kwa furaha na kumkaribisha mgeni nyumbani. Noel ni kipindi cha kutembeleana, kupeana zawadi na kufurahiana.
Mama Maria baada ya kuambiwa na Malaika Gabrieli kuwa ana baraka, (mja mzito), akaondoka mara moja kwenda kumtembelea ndugu yake Elizabeti aliyekuwa na baraka ya Yohane mbatizaji. Ndivyo tunavyosali katika fumbo la pili la rozari ya furaha: “Uliyekuchukua ulipokwenda kumtazama Elizabeth.” Aliwasili huko, Maria akamwamkia Elizabeth na kuendelea na mazungumzo. Lakini mazungumzo ya akina mama hawa ni tofauti. Hawa wanaongea lugha ya utaalamu wa hali ya juu wakinukuu Agano la kale kama vile unasikiliza mhadhala wa Wataalamu wa Biblia. Kwa hiyo, ili kuupata ujumbe wa mazungumzo ya akina mama wa leo, yakubidi ukae mkao wa nidhamu na kuwasikiliza kwa nidhamu, vinginevyo utatoka kapa.