WAKATI
mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Yanga, wakitarajiwa kushuka
kwenye dimba la Mkwakwani jijini Tanga kuwavaa wenyeji Coastal Union ‘Wagosi wa
Kaya’ leo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limewataka mashabiki
watakaosafiri kwenda huko kuhakikisha wanakamilisha kununua tiketi za
elektroniki.
Yanga iliyotoka kusaka makali
nchini Uturuki inajitupa Mkwakwani
kuwavaa Wagosi wa Kaya waliotoka kusaka mavumba Oman, katika pambano
linalotabiriwa kuwa na ushindani na kuvuta mashabiki wengi kutoka Dar es
Salaam, Morogoro na Arusha, ambapo TFF imewataka kuhakikisha wanaepuka usumbufu
kwa kusafiri wakiwa na tiketi zao mkononi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana,
Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, alisema kuwa mauzo ya tiketi za mechi
hiyo yalianza juzi na ni vema mashabiki hao wakanunua watokako, kuliko
kutarajia kwenda kununulia Tanga.
“Uzoefu unaonyesha kuwapo kwa mambo yanayochangia usumbufu
katika ununuzi wa tiketi za elektroniki, hivyo tunawaomba mashabiki wa Dar,
Morogoro na Arusha ambako vituo vya mauzo vipo, kununulia huko, kuliko
kutarajia kwenda kununulia kule,” alisisitiza Wambura.
Aliongeza kuwa TFF, Bodi ya Ligi na wazabuni wa mfumo mpya wa
tiketi hizo, benki ya CRDB, wanatambua uwepo wa changamoto miongoni mwa
mashabiki katika kuuelewa, lakini akasisitiza kuwa wako tayari kukabiliana nazo
kwa kutoa elimu kuliko kuufuta.
“Tunatambua ugumu uliopo, ndiyo maana tunawaomba wadau wetu
kuhakikisha wanajifunza taratibu na hatimaye wataelewa na kuutumia vizuri. Kwa
sasa msisitizo wetu ni kuwa mashabiki wasio na tiketi wasiende viwanjani, kwani
haziuzwi huko,” alisema Wambura.
Alitaja viingilio katika pambano kati ya Coastal na Yanga kuwa
ni sh 5,000 na 15,000, kwa tiketi moja zinazopatikana kupitia M-Pesa, CRDB
SIMBanking na CRDB Fahari Huduma.
Mechi nyingine zitakazopigwa leo, Ruvu Shooting watakuwa wenyeji
wa Mbeya City Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani, ambako viingilio ni sh
10,000 na sh 5,000 huku Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, Kagera Sugar
watawaalika wakata miwa wenzao, Mtibwa Sugar ya Manungu Turiani, Morogoro,
viingilio vikiwa ni sh 5,000 na 3,000.
Nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, kule Chamazi Mbagala, Azam
FC watakuwa nyumbani Azam Complex kuumana na Rhino Rangers ya Tabora, viingilio
vikiwa sh 10,000 na 3,000
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni