Week Hot newz

Historia ya Kanisa la Sabato (4)

NDUGU yangu, ninatumaini nimekufikisha mahali pazuri. Hiyo ndiyo historia ya mshazari wa Kanisa la Wasabato. Kifupi haina mashiko na mtiririko wa kimantiki. Hata hivyo baada ya kuzaliwa kimtindo namna hiyo, Kanisa la Wasabato halikubaki moja kifikra na kimtazamo. Ukilichungulia ndani, Kanisa la Wasabato ni Muungano wa Vikundi vitatu vya Waadventisti; Kikundi cha Bw. Hiram Edson, kilichosisitiza zaidi mafundisho ya huduma ya Yesu Patakatifu pa Patakatifu mbinguni, Kikundi cha Bw. Joseph Bates, kilichosisitiza zaidi kufuata Sabato ya Agano la Kale na Kikundi cha Bi Ellen G. White, kilichomwona Bi Ellen kama nabii ambaye unabii wake ni lazima ufuatwe na Waadventisti wote duniani. Vikundi hivi vilipoungana Waadventisti Wasabato wakapata kujichipusha duniani. Mwaka 1860, Jina la Seventh Day Adventist lilichaguliwa nalo likawa jina rasmi la Waadventisti hao. Mei, 1863, katika mkutano mkuu wa kwanza, uliokuwa na wawakilishi kutoka majimbo yote Marekani, isipokuwa jimbo la Vermont, kanisa la Wasabato likazaliwa rasmi duniani. Kwa vyovyote kanisa la Wasabato halikubaki moja isipokuwa liliendelea kumegekamegeka kiasi kwamba leo hii kuna zaidi ya makundi hamsini ya Wasabato duniani. Ndugu yangu, niache nikomee hapa hapa. Bila shaka, niliyoyasema yanatosha Muhtasari Basi, tukipiga muhtasari wa historia ya Wasabato, tuseme tu kwamba Mwasisi wa Waadventisti Bw. William Miller (1782-1849) alikuwa ni mkulima Mbaptisti wa Massachusetts. Yeye alifuatiwa na Bw. Joseph Bates aliyeliamsha wazo la Wakristo kurudi kwenye Sabato ya Wayahudi ambaye alikuwa bado Mbaptisti. Lakini hatimaye mshamirishaji mkubwa wa Usabato yaani Bi Ellen G. White alikuwa ni Mmethodisti. Hatimaye, kwa kuhitimisha sehemu hii, yafaa sote tukumbuke kwamba makanisa hayo mawili, yaani Wabaptisti na Wamethodisti si chochote isipokuwa matawi ya Kanisa la Anglikana, kanisa lililoanzishwa na Mfalme Henry VIII wa Uingereza hapo mwaka 1534 baada ya kukasirika kukataliwa na Kanisa Katoliki kumwacha mkewe aliyeshindwa kumzalia mtoto wa kiume. Jumla ya yote haya ndiyo chuki ya Wasabato inayorindima hadi leo hii hata sisi sote kunyanyasika, pasipo kuwakosea lolote. Lakini nimeshakuonesha kwamba wameibukia kwenye fedheha ya kutokutimia kwa utabiri wa siku ya mwisho wa dunia na kutoka hapo wamekuwa wakigeuka geuka kwa tikitaka nyingi za kindoto ambazo kwazo hawakuwa na haki kutunyanyasa watu tuliobaki kwenye ukweli wa Agano Jipya. Hayo ndiyo yanayoitwa majanga, kukosea akosee kiongozi wao kutukanwa tutukanwe sisi. Si ajabu hiyo? Basi, si kitu, tudumu katika mema na Kanisa letu jema. Uamuzi wetu tulioufanya si wa kujutiwa. Sisi tunamfuata Yesu Kristo ambaye tumeagizwa tumsikilize na si mtu yeyote ambaye anataka kupotosha ukweli wa Kanisa Katoliki (rej. Mk 9:7). Wewe basi fanya uamuzi sasa, je unataka kuwafuata watu wanaoficha historia yao ya aibu au unataka kumfuata Yesu kweli kweli? Mimi mwenzio sidanganyiki, labda wewe. Lakini lisingelikuwa jambo la hekima katika karne hii ya ishirini na moja. Hii si karne ya kudanganyika wala ya kubaki katika limbikizo la uongo. Amka usibaki gizani. Funguka na ukweli huu mpya. Yesu alikuja kutukomboa (rej. Luka 4:18-19). Wasabato wanaolitusi Kanisa wanaweza kuitwa Mitume wa Matusi Dhidi ya Kanisa la Kweli. Msomaji wangu, bila shaka umeiona historia ya na zigzaga ya Wasabato. Wenyewe wanaificha sana historia hiyo, hasa kwa wafuasi wao wanaoingia katika kanisa lao ili wasijue undani wao. Wanakatazana kusoma vitabu vilivyoandikwa na wasio wasabato na hata jibu kama hili hawaruhusiwi kulisoma. Wanaogopa ukweli kutoka nje. We acha wafiche, lakini sisi tunajua na leo nimekuambia ukweli kuhusu historia yao! Umeshaona? Kifupi historia yao isiyoeleweka ipo katika mizizi mitatu. Mosi, mambo yameanzia kwenye kuthubutu kutabiri tarehe, siku na saa ya mwisho wa dunia, mambo yasiyoweza kutabirika na mwanadamu yeyote. Pili, mafundisho mengine yamejengwa kwenye ndoto za kuota kuweko kwa hekalu mbinguni, wakati Maandiko Matakatifu yanasema mbinguni hakuna hekalu. Hatimaye, tatu, ndoto na mafundisho yenyewe yanapingana na Bwana wa Ukristo. Yesu alifundisha amri kuu ni upendo, wakati waota ndoto hao wanasema ni kuishika sabato. Wao wanasema hayo kama nani? Kama huo si upinga Kristo ni kitu gani, ndugu yangu msomaji? Hivi ndugu zangu wanachuo wa Chuo cha Udaktari, KCMC, Moshi na wasomaji wengine wote, kile mlichosikia kwamba Kanisa la Sabato lilianza kwa kufunika aibu ya utabiri wa tarehe ya mwisho wa dunia ambao haukutimia ni kweli kabisa. Historia ya Kanisa la Sabato ndiyo hiyo niliyowadadavulia ijapokuwa labda kwa ufupi tu. Ipuuze, ni historia ya aibu na ndiyo kisa inafichwa. Yaani kama ulivyonifuatilia, ni historia isiyo na kichwa wala miguu, achana nayo kabisa. MWISHO Mwandishi ni Padri, Mtaalamu wa Biblia na Gombera wa Seminari Kuu ya Peramiho iliyopo katika Jimbo Kuu Katoliki la Songea

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni