Week Hot newz

Magufuli amwaga mkwara kanisani


Rais Dk. John Magufuli, akiwa na Waziri Mkuu mstaafu wa Kenya, Raila Odinga, katika Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato mkoani Geita jana. PICHA: IKULU
Rais John Magufuli,  amesema atahamishia utumbuaji majipu kwenye Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato mkoani Geita, endapo mchango wa Sh. milioni 10 aliotoa kwa ajili ya upanuzi wa kanisa hilo zitatumiwa vibaya.

 
Rais Magufuli ambaye jana alishiriki ibada ya asubuhi katika kanisa hilo akiwa na Waziri Mkuu mstaafu wa Kenya, Raila Odinga, aliahidi kuchangia Sh. milioni 10 kwa ajili ya upanuzi wa Kanisa.
 
Baada ya ibada hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msingwa, alitoa taarifa kwa vyombo vya habari akisema fedha alizoahidi Rais aliposali misa ya kwanza, zimekabidhiwa kanisani hapo wakati wa misa ya pili na Naibu Mnikulu, Ngusa Samike.
 
MAGUFULI KANISANI
Wakati wa misa ya asubuhi, Paroko wa kanisa hilo, Padri Mlinganisha Mwilinde, alimtaka Rais Magufuli kuwasalimia waumini wenzake kwani tangu alipochaguliwa mwaka jana kuwa Rais, hakuwa amekutana nao.
 
Alipokuwa akisalimia, Rais Magufuli alisema: "Nimesikia kwenye matangazo kuwa mnahitaji kukamilisha ujenzi wa kanisa hili…na mimi niwaahidi kuwa nitatoa Shilingi milioni 10…hizi nina uhakika nazo nikirudi Dar es Salaam, nitazituma…tena nitaziwahisha ili ikiwezekana ndani ya wiki moja ziwe zimefika," alisema Rais Magufuli na kuongeza:
 
"Ila niwape tahadhari. Fedha hizo zitumike vizuri na nitafuatilia ili kujua zimefanya nini, vinginevyo nitawatumbua humu ndani ya Kanisa." 
 
"Lazima na mimi nichangie maana hapa ni kwetu na hata nikifa nitaletwa kuzikwa Chato…hata wakati nikiwa mdogo, nilikuwa mtumikiaji hapa hapa kanisani," alisema.
 
Awali, aliwataka waumini wote kushikamana na kuacha kutengana na kubaguana kutokana na itikadi za kisiasa, ukabila na dini kwani wote ni Watanzania na wajikite kudumisha amani, upendo na mshikamano.
 
Hata hivyo, alimwelezea Odinga pamoja na familia yake kuwa ni marafiki wake wa karibu na kwamba amewahi kuja Chato kumsalimia awamu mbili ikiwamo wakati wa mazishi ya baba yake, marehemu Joseph Magufuli.
 
"Baba Paroko, kama utaniruhusu niombe pia kumtambulisha rafiki yangu kwelikweli aliyelazimika kutoka Kenya kuja Tanzania baada ya kusikia nipo nyumbani kwetu Chato.
Ni rafiki yangu wa ukweli kwani urafiki haujali nchi, kabila, chama wala rangi ya mtu…amekuja jana kunisalimia na yeye amelala kijijini kwetu Rubambangwe," alisema na kuongeza:
 
"Huyu rafiki yangu amekuwa mtu wangu wa karibu sana…amenisaidia mambo mengi…kwa kuwa leo tupo hapa Chato, naomba na yeye mumuone kwani ni mtoto wenu."
 
ODINGA
Akizungumza na waumini waliokuwa kanisani hapo, Odinga  aliweka wazi siri ya ukaribu wake na Tanzania, akisema alikwenda kusoma nje ya nchi yake baada ya kutumia hati ya kusafiria ya Tanganyika.
 
Odinga aliyekuwa ameongozana na mkewe pamoja na binti yao, Winny Odinga, alisema hatua hiyo ilitokana na uhusiano mwema kati ya Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere na baba yake (Odinga), Jaramogi Odinga.
 
"Wakati nikiwa mdogo na Kenya ikiwa bado inatawaliwa na wakoloni, Baba yangu alitaka niende ng'ambo, lakini wakoloni hao waligoma kabisa kunipa passport (hati ya kusafiria)… kilichofuata baba yangu Jaramogi, alinituma Tanzania nikaja kuonana na Mwalimu Nyerere ambaye ndiye aliyenipa passport ya Tanganyika nikafanikiwa kwenda ng'ambo," alisema na kuongeza:
 
"Kwa mantiki hiyo, unaweza kuona mimi nilivyo ndugu yenu…kikubwa ninachoweza kusema hapa ambacho pia padri alikikazia, ni kukuomba Rais Magufuli umwombe Mungu akupe hekima kama mtumishi wa Mungu Selemani alivyochagua."
 
"Kungoza taifa ni kazi ngumu na kwamba katika nafasi yako utakutana na majaribu mengi kama aliyokutana nayo Yesu kule mlima wa Yeliko…lakini inapotokea; sema toka shetani," alisema Odinga.
 
Ondinga ambaye ni Waziri Mkuu mstaafu na mpinzani wa karibu wa Rais Uhuru Kenyatta, anatajwa kuwa atawania nafasi ya urais wa nchi hiyo mwakani.
 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni