Tunaendelea katika safari yetu ya
tafakari masomo Dominika ya nne ya kipindi cha mwaka. Neno la Mungu
latualika kuwachagua maskini. Katika kuwachagua maskini yatulazimu kuwa
maskini wa roho tukitambua kuwa ufalme wa mbinguni unajifungamanisha na
heri hiyo.
Katika
somo la kwanza, Nabii Sefania anawaalika walio wacha Mungu, kutafuta
daima haki na unyenyekevu, maana ni kwa njia hiyo katika siku ya hukumu
Mungu atawahurumia. Anasema kwa hakika wale wote walioonewa na
kutumainia jina la Mungu watabakizwa na hawatasahauliwa kamwe.
Nabii
Sefania anakuja na mahubiri haya akisukumwa na hali ya maisha ya wakati
wake katika kipindi kabla ya uharibifu wa Hekalu la Yerusalemu, na hasa
mawazo juu ya mali. Katika kipindi hicho mali ilikuwa ni kipimo cha
baraka toka kwa Mungu. Aidha, mtu alionekana kuwa wa maana kwa kuwa na
mali. Basi Nabii Sefania na Manabii wengine, wanaona wakati fulani mali
hupatikana kwa sababu ya unyonyaji wa maskini, na hivi wanaanza kukemea
hali hiyo. Umaskini haukuwa tokeo la dhambi, bali tokeo la madhulumu
toka kwa matajiri.
Nabii Sefania anakemea kwa nguvu zote jambo
hili pamoja na kwamba alikuwa amezaliwa toka familia tajiri. Anawaalika
watu kutambua ujio wa adhabu ya Mungu kama wataendelea na unyonyaji kwa
maskini. Ndiyo kusema anawaalika kurudi kwa Mungu kwa njia ya toba na
kutenda haki. Nabii anaona kufanya toba lazima kujikite katika kuwa
maskini wa roho, kuwa wanyenyekevu daima kama karama msingi kwa ajili ya
maisha ya kumpendeza Mungu.
Kwa njia ya Nabii tunatambua, nini
maana ya umaskini wa roho, kumbe si hali ya mtu au nafasi ya mtu katika
jumuiya bali njia ya kiroho, hali ya ndani ya mtu anayetafuta wokovu.
Umaskini wa roho ni kutokuwa na hali ya kujitegemea na kwa namna hiyo
kumtegemea Mungu. Ndiyo kusema, mwaliko kwetu hivi leo ni kutafuta namna
ya kujinasua toka mali kwa ajili ya uzima wa milele.
Katika somo
II toka barua ya Mt. Paulo kwa Wakorinto tunamwona Mungu anavyochagua
mambo dhaifu ili kuaibisha wenye hekima. Mungu anachagua maskini wa roho
badala ya wanaojigamba. Kumbe Paulo anawaalika Wakorinto waliochaguliwa
na Mungu kwa njia ya Kristo, hekima ya Mungu, haki na shime yao kuwa
makini katika hilo. Kwa nini Paulo anakuja na fundisho hili? Ni kwamba
jumuiya ya Wakorinto ilijawa na utengano kwa sababu ya madaraka na
utajiri. Utengano huu ulileta maudhi hasa kwa maskini!
Mt Paulo
sasa anawaonya kwa maneno makali na hata yanayoweza kufanya mtu afikiri
kuwa hekima si ya maana. Hekima na akili ni vya maana lakini lazima viwe
kwa ajili ya huduma kwa watu na kwa Mungu. Mungu anachagua maskini na
si fukara, kumbe umaskini wa roho, unaojali maisha ya watu na kumweka
Mungu katikati ya safari ya wokovu wa wanajumuiya wanaoishi na kusafiri
pamoja wakielekea mbinguni.
Katika somo la Injili, toka Injili ya
Matayo, tunapata kutafakari Heri Nane za mlimani. Kwa kifupi Heri Nane
ni ufupisho wa mafundisho mazima ya maisha ya kiroho na mwongozo wa
namna ya kufika mbinguni. Mungu anawachagua walio maskini wa roho, yaani
wale ambao huweza kuchagua njia ya unyenyekevu, huruma, msamaha,
furaha, haki, utakatifu, amani, uvumilivu wakati wa taabu itokayo na
utafutaji wa haki pamoja na taabu itokayo na dhuluma, kama ndio warithi
wa uzima wa milele.
Mpendwa, yafaa kujiuliza, hivi Mungu apendezwa na
umaskini? Mbona Injili yatualika kufanya bidii ili kuondoa umaskini
katika maisha yetu? Ni kweli, Mungu hapendezwi na umaskini bali
apendezwa na umaskini wa roho ambao huleta wokovu. Kuhusu mali, Bwana
hatofautiani na manabii waliomtangulia, yaani haoni mali kama alama ya
baraka toka kwa Mungu, lakini pia habezi mali. Sasa ataka nini!
Yafaa
twende kuangalia neno mali kama lilivyotumiwa na Matayo na matumizi ya
mali tuliyonayo! Tukitazama Injili ya Lk 16:9 tunaona neno mali hupata
maana sahihi kiroho pale tunapogawanya mali hiyo kwa maskini. Hata hivyo
Bwana huona hatari itokanayo na mali tunapoelekea mbinguni, angalia Lk
14:33 akisema hakuna anayeweza kuwa mfuasi wangu kama atashikama na
mali. Fundisho la Bwana latudai kujibandua toka mali ili kumfuasa yeye
na ndio msingi wa kuweza kuelewa nini maana ya kuwa maskini wa roho.
Mpendwa
msikilizaji, mwaliko katika fundisho ni kujipatia uwezo wa
kushirikishana mali tulizojaliwa na Mungu. Bwana hapendezwi na ufukara
ambao huja bila kuchagua bali hupendezwa na umaskini ambao mtu
anauchagua kwa ajili ya huduma ya Injili. Ndiyo kusema furaha kwa wale
wanaochagua umaskini kwa ajili ya kujitoa kwa waliowahitaji ni tele na
ya uhakika. Umaskini mwingine tofauti na huo si heri na si njia ya
kiroho bali njia ya uvivu na kwa hivi hakuna furaha. Aidha umaskini wa
roho unaokuja kwa njia ya uchaguzi wa ndani katika mlengo wa Injili ni
mwito kwa ajili ya wakristu wote na si kwa tabaka fulani kati ya
waamini.
Tukiitazama heri II yaani wanaheri wale wenye huzuni,
tunapata kujiuliza swali, je Mungu apendezwa na huzuni? Kwa hakika
hapana, kumbe heri hii ni kwa wale ambao wanahuzuni kwa sababu wanateswa
kwa ajili ya imani yao. Heri inakuja kwa maana hali yao hiyo
itaondolewa na watafarijiwa, na Mungu. Bwana akisonga mbele anatangaza
tena heri kwa walio wapole maana watairithi nchi. Wapole ni wale
wastahimilivu na wanyenyekevu. Bwana hasifu unyenyekevu na uvumilivu wa
asili, yaani zawadi za Mungu kwa mtu tangu kuzaliwa kwake bali asifu
upole na uvumilivu wa kiroho ambao mtu hujipatia mbele ya madhulumu ya
haki zake, akionesha uvumilivu, akimtegemea Mungu pasipo kupambana kwa
njia ya vita!
Mpendwa, katika msingi uleule wa upole Bwana
anatangaza heri kwa wenye njaa na kiu ya haki kwa maana watashibishwa.
Kwa heri hii, ataka tutambue na tupiganie haki kwa ajili ya wote kama
ambavyo mtu hutafuta chakula kwa ajili ya kuishi. Ndiyo kusema, kama
ilivyo njaa ya chakula basi ijengeke njaa na kiu ya haki. Mpendwa
msikilizaji, Bwana anasonga mbele akitangaza heri wenye huruma, akitaka
tuwe na huruma, huruma ambayo hujihusisha katika kuwasaidia wengine,
yaani isiyoishia katika kusamehe bali katika kuhakikisha wengine
wanapata kuishi na kuokoka. Heri hii inakuja kwa maana ufalme wa Mungu
utakapokuwa umetimia nao watapata mmojawapo wa kuwasaidia na kuwafariji.
Kristu katika hili anatangaza maisha mpya ambamo ubinafsi na magomvi si
vitu vya maana bali mapendo na rehema kwa wengine.
Bwana
anasonga mbele katika mafundisho yake akikazia usafi wa moyo kama kigezo
cha kuweza kumwona Mungu. Katika heri hii, Bwana hazungumzii useja bali
unyoofu na ukweli unaomfanya mtu asihangaikie fikira potofu kinyume na
mapenzi ya Mungu. Huyu mwenye usafi wa moyo hagawanyi upendo wake na
maisha yake kwa wafalme wawili yaani Mungu na shetani bali tu kwa Mungu.
Ni kwa jinsi hiyo basi moyoni mwake hukaa mawazo na mapendo ya kimungu
ambayo ndiyo umletea heri na furaha daima. Kilele cha heri hii ni
kumwona Mungu.
Katika mambo msingi ambayo mwanadamu anayahitaji
ni amani. Amani ni tunda la Roho Mtakatifu. Ni tokeo la kuzaliwa Mwana
wa Mungu, kumbuka utukufu kwa Mungu juu na amani duniani kwa watu wenye
mapenzi mema. Bwana anatangaza heri kwa watenda na watafuta amani, yaani
wapatanishi kwa ujumla. Neno amani katika Biblia halina maana tu ya
kutokuwepo kwa vita bali hulenga ustawi wa watu, haki, furaha, afya
njema na maisha maelewano. Mpendwa msikilizaji, maisha ya namna hii
hujengwa na hivi Bwana anatangaza heri na baraka kwa wale
watakaojishughulisha na ujenzi wa amani katika taifa la Mungu.
Mpendwa
msikilizaji, Bwana akimalizia mafundisho yake pale mlimani anakuja na
tangazo la heri kwa wale ambao katika kutenda heri hizi na hasa
wakitafuta haki wataudhiwa na kudhulumiwa, akisema ufalme wa mbinguni ni
wao. Kwa hakika awaye yote anayetafuta kutenda haki, atadhulumiwa na
kunyanyaswa. Ndiyo kusema wadhulumaji huogopa ujio wa ukombozi na hivi
kujiweka katika mapambano kinyume na ufalme huo. Bwana akijua hilo
anatangaza heri kwa awaye yote atafutaye amani yakwamba akibaki imara
atapata furaha na baraka za Mungu.
Tukumbuke pia kwamba, Bwana
aliteswa, lakini alivumilia kiasi kwamba Mungu akamwadhimisha mno na
kumpa jina lipitalo kila aina ya jina. Mpendwa, kupokea heri za Mungu
si jambo jepesi, ladai kuzama katika maisha ya kiroho ili polepole
kukuza roho ya mapendo na utii kwa Mungu. Tunaitwa kuwa watakatifu kama
Baba yetu aliye mbinguni.
Mpendwa mwana wa Mungu nikutakie baraka na heri za mbinguni sasa na daima na milele. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C. PP.S.